BALOZI SEIF AHIMIZA MAZOEZI

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba Jamii inapaswa kuzingatia ulazima wa kufanya mazoezi ya Viungo kila mara ili iweze kujenga afya njema na hatimae kupunguza gharama za matibabu kwa magonjwa yanayoweza kutibika.

Alisema kulingana na mabadiliko ya mifumo ya Afya na Ulaji wa vyakula vya kutengeneza visivyozingatia utaratibu wa Kitaalamu Duniani kote mazoezi yanalazimika kupewa kipaumbele kikubwa katika kuimarisha Afya za Wanaadamu.

Balozi Seif Ali Iddi alisema hayo mapema asubuhi wakati wa Bonaza la Vikundi vya Mazoezi  Nchini lililoandaliwa na kikundi cha New Life Exercise Club na kile cha Kiembe Samaki Fitness Club na kufanyika katika Uwanja wa Amaan Mjini zanzibar.

Alisema mazoezi ni sehemu pia  inayowafanya Watu kuondokana na mihemko na kuachana na mawazo ya kufanya vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia. Hivyo ametoa wito kwa wanamichezo hao kuwa Mabalozi wa Kampeni ya kuwahimiza watu wafanye mazoezi, kupinga udhalilishaji, kuchangia damu pamoja na kupiga vita dawa za kulevya.

“ Napenda nisisitize kuwa mazoezi kama hayo yatumike katika kuhamasisha Jamii ya Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla ili waweze kuepukana na maradhi tofauti”. Alisema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Balozi Seif alielezea kwamba anatambua changamoto zinazovikabili vikundi vya mazoezi Nchini lakini bado wako pamoja na Serikali yao katika kuhakikisha kwamba wanaendelea kuhamasisha watu kufanya mazoezi sambamba na kuchangia  damu jambo ambalo ni muhimu katika kuokoa maisha ya Watu.

Alitoa wito kwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo kushirikiana na Uongozi wa Vikundi vya Mazoezi katika kuona changamoto ndogo ndogo zinazowakabili zinapatiwa ufumbuzi.

Balozi Seif alisema ni vyema ushiriki wa sehemu hizo mbili ukasaidia jinsi ya kuboresha mazoezi hasa kwa kuvipatia Elimu Vikundi vya Mazoezi ili wanamichezo wao waweze kwenda na wakati kwa kufanya mazoezi yenye tija kwa Afya zao.

Balozi Seif aliwapongeza Viongozi wa Vikundi vya New Life Exercise Club na Kiembe Samaki Fitness Club kwa jitihada zao katika kuwaunganisha na kuwaweka pamoja wana vikundi vya mazoezi.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwasisitiza wanavikundi na wanamichezo pamoja na mazoezi wanayofanya, wasiache kupima afya zao kila mara ambako kunaweza kusaidia kuepusha vifo vya Ghafla.

“ Kupima Afya ni muhimu sana, hasa Virusi vya Ukimwi, kisukari, maradhi ya Moyo, tezi dume kwa wale wenye umri ulipindukia wa Miaka 55. Kuna maradhi yakigundulika mapema yanatibika”. Alisema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Balozi Seif alisema jamii imeshuhudia mara nyingi kuona vifo vya ghafla vinavyotokea Mitaani ambavyo historia yake inapogundulika hubaini kwamba marehemu hakuwa na tabia ya kupima afya pengine alikuwa na ugonjwa kwa muda mrefu usiojuilikana mapema.

Akitoma Risala mwakilishi wa Vikundi vya mazoezi vya New Life Exercise Club, Kiembe Samaki Fitness Club na Hits FM  Kudra Mawazo  alisema Bonaza hilo lililoasisiwa Mwezi Disemba Mwaka 2017 limebeba dhana nzima ya Kampeni Maalum ya kupinga udhalilishaji wa Kijinsia unaoonekana kushamiri katika Mitaa mbali mbali Nchini.

Kudra alisema Siku 16 zilizotengwa Maalum kwa ajili ya Kampeni hiyo zimesaidia kuwaunganisha Wanamichezo katika pembe zote za Zanzibar kujenga Uzalendo unaosaidia  kuunganisha nguvu za kukabiliana pia na Dawa za Kulevya Visiwani Zanzibar.

Hata  hivyo Kudra Mawazo alielezea changamoto kadhaa zinazovikabili Vikundi mbali mbali vya Mazoezi Nchini akizitaja baadhi kuwa ni kufanya mazoezi katika Viwanja vya kukodi pamoja na ukosefu wa Vifaa na Jezi za mazoezi.

Mapema Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi Ayoub Mohamed Mahmoud  alisema Kampeni Maalum ya kupinga udhalilishaji wa Kijinsia iliyoanza kuchanja mbuga mara baada ya Dua ya kuliombea Taifa kuwa na Amani Mwezi Disemba Mwaka 2016 imeanza kufahamika miongoni mwa Wananchi.

Alisema Serikali ya Mkoa Mjini Magharibi inaendelea kuchukuwa hatua za kupinga udhalilishaji zinazoibuka na kuhusisha zaidi vyanzo vya maeneo ya Starehe kama Baa, Miziki ya usiku pamoja na michezo isiyozingatia Maadili na Tamaduni za Taifa.

Mkuu huyo wa Mkoa Mjini Magharibi alionya na kutahadharisha wazi kwamba Serikali haitamuonea haya au kumuogopa Mtu ye yote kwa sababu ya Umaarufu, cheo au Ujanja atakaotumia katika kufanya vitendo vya kudhalilisha Watu hasa Wanawake na Watoto wasiyo na hatia ye yote.

Ayoub aliahidi kuwa Serikali kupitia vyombo vyake vya Dola  itaendelea kulinda raia zake wote katika misingi ya usawa pamoja na kuwaepusha na changamoto za vitendo vyovyote vilivyo nje ya maadili, Sheria na Taratibu zilizowekwa.

Mapema asubuhi Wanamichezo hao kutoka Vikundi mbali mbali Mjini na Vijijini walifanya Matembezi yaliyoanzia viwanja vya Komba Wapya, kwa kupitia Biziredi, Muambe Ladu, Mikunguni,  Kwawazee na kushia Uwanja wa Amaan.

Katika Bonaza hilo liloshirikisha michezo mbali mbali ukiwemo ule maarufu wa kuvuta Kamba pamoja naUmahiri mkubwa uliyoonyeshwa na Binti Mdogo wa Miaka 10 Ahlan Saleh kwa kucheza Mchezo wa Yoga.




Othman Khamis Ame

Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

24/2/2018.

Comments

Popular posts from this blog

HUYU NDIYE MCHEZAJI MWENYE REKODI YA KUFUNGA MAGOLI MENGI KWENYE MECHI YA TAIFA DHIDI YA BOYS