ZANZIBAR YAZIDI KUNG’ARA UMISSETA, INAONGOZA MAKUNDI YAO


TIMU za Zanzibar zimeendelea kufanya vyema katika michezo yake mbali mbali iliyocheza leo, baada ya kuibuka na ushindi na kuleta matumaini makubwa ya kuingia hatua ya robo fainali kwenye Mashindano ya Michezo na Sanaa kwa Skuli za Sekondari Tanzania (UMISSETA) yanoyoendelea katika Viwanja vya Chuo cha Ualimu Butimba, Mwanza.

Katika michezo iliyopigwa leo, upande wa Soka timu ya Unguja imefanikiwa kuondoka na ushindi wa bao 1-0 dhidi Morogoro, mchezo ambao ulikuwa mkali na kuvutia kwa muda wote.

Katika pambano hilo, licha ya kufungwa Morogoro walionesha kiwango kizuri na kuwabana Unguja ambapo hadi kipindi cha kwanza kinamalizika cha hakuna timu iliyoweza kuona lango la mwenzake.

Kipindi cha pili timu zote zilirudi na nguvu mpya kila mmoja akitaka kupata bao la mapema, lakini bahati hiyo iliwaangukia Unguja baada ya kuandika bao hilo pekee lililokwamishwa wavuni dakika ya 72 kupitia kwa Ali Hassan (Ndimbo).

Mchezo mwengine uliwakutanisha kanda ya Pemba ambayo ilikuwa na kazi ya kupepetena na mkoa wa Singida, pambano ambalo lilimalizika kwa Pemba kuibuka na ushindi wa bao1-0 dhidi ya Singida bao ambalo lilifungwa na mchezaji Mohamed Ali ndani ya dakika ya 15.

Kwa upande wa mchezo wa mpira wa Mikono (Handball) timu ya kanda ya Unguja imefanikiwa kuondoka na ushindi wa mabao 22-2 dhidi ya Mtwara.
Kumalizika kwa michezo hiyo tumezungumza na captain wa soka Unguja Ibrahim Ali (Chafu) na wa Pemba Abdul latif Said Masoud wamesema kutokana na maandalizi waliyoyafanya wataendelea kutesa kwenye Mashindano hayo.

Timu ya Soka ya Kanda ya Pemba inaongoza kundi lao B wakiwa na alama 9 baada ya kushinda michezo yote mitatu kufuatia mchezo wa awali kuwafunga Mabingwa watetezi Songwe 1-0, kisha jana kuwachapa Shinyanga bao 1-0 na leo kuwamaliza Singida 1-0 hivyo wamecheza michezo mitatu mfululizo bila ya lango lao kuruhusu kufungwa hata bao moja.

Unguja wao wapo kundi D wanaongoza pia kufuatia kushinda yote miwili na kuwa na alama sita baada ya mchezo wa kwanza kuwafunga Mtwara mabao 2-1 na leo kuwachapa Morogoro bao 1-0 ambapo kesho saa 2:00 za asubuhi watakuwa na mchezo wao watatu kucheza na Njombe.

Comments

Popular posts from this blog

HUYU NDIYE MCHEZAJI MWENYE REKODI YA KUFUNGA MAGOLI MENGI KWENYE MECHI YA TAIFA DHIDI YA BOYS